MAMBO 5 YA KUFANYA KABLA YA KUACHA KAZI NA KUJIAJIRI




Kama uko kwenye ajira sasa na unatamani kujiajiri ni vema ukizingatia mambo yafuatayo kabla hujaamua kuacha kazi :

1. *Tengeneza chanzo/vyanzo vya pesa nje ya mshahara*. Ni muhimu sana kama uko kwenye ajira na unawaza kuja kuachana na ajira kuanza leo kufikiri kuanzisha vyanzo vya mapato nje mshahara wako wa kila mwezi .
Siri ni hii kwamba ukiwa na chanzo kingine cha fedha kitapunguza hofu ya maisha yako baada ya kuacha kazi maana utakuwa na uhakika wa kupata mahitaji yako ya msingi  hata kama mshahara haupo.

Watu wengi wameshindwa kuacha kazi japo wanatamani kuacha kazi kwa sababu vipato vyao vinatokana na chanzo kimoja na hivyo  wanaogopa wakiacha kazi ghafla familia yake itayumba.Fikiria ni biashara gani unaweza fanya wakati uko kwenye ajira bila kuathiri kazi yako .Angalia ni kwa namna gani unaweza kuanzisha mradi wowote eneo ulipo na kama una mashamba fikiria hata kuanzisha kilimo na ufugaji .

2. Tafuta Taarifa sahihi : Ni muhimu sana kuwa na taarifa sahihi juu ya kile unachofikiri kufanya baada ya kuacha kazi kinyume na hapo unaweza kuangukia sehemu ambako siko na ukawa umepoteza muda na rasilimali  nyingi .Unashauriwa kutumia muda mwingi ukitafuta undani wa kile unachotaka kukifanya.Hii ni pamoja na kujua mtaji unaohitajika ,Masoko ,wataalam n.k

3. Andika Mchanganuo wa kibiashara : Ni muhimu sana ukiwa bado uko kazini kuanza kufanya mchanganuo wa mradi unaotaka kufanya .Mchanganuo huu hutoa picha ya mtaji ,masoko ,watu wanaohitajika ,washindani na mambo mengine kama hayo .Kama huwezi kuandika waone wataalam wakusaidie .Umuhimu wake ni kwamba taasisi nyingi za fedha na watu wanaoweza kukusaidia kupata fedha ya mradi wako wanahitaji mchanganuo huo .

4. *Anza kujifunza Usimamizi wa biashara: Ni muhimu sana kupata elimu ya kutosha juu ya biashara na kwa sasa teknolojia ilivyofika mbali ni rahisi kujifunza kwa kutumia mtandao .Tumia muda mwingi kujifunza kuhusu biashara na usimamizi wake kwa kusoma vitabu vya biashara na video ambazo zinaelekeza namna ya kufanya biashara .Acha kabisa uvivu wa kutokupenda kusoma kama kweli unataka kujiajiri .

5. *Acha Uvivu* :Kama unajua kabisa wewe ni mvivu kwenye kazi Za watu na mambo yako binafsi tafadhali usiwaze kujiajiri maana kujiajiri wewe ndiye mratibu wa kila kitu kwa hiyo muda mwingi itakubidi ufanye kazi .Anza kujibidiisha na kuacha uvivu usio na maana .Jifunze kufanya kazi bila kusukumwa maana ukiwa kwenye mambo yako hakuna atakayekusukuma .Utafiti wangu usio rasmi umegundua kuwa watanzania wengi hawapendi kujiajiri kwa sababu ni wavivu na hawawezi kujisimamia