UWAJIBIKAJI NDIO UTAMALIZA TATIZO LA AJIRA






Dunia sasa inakumbwa Na janga kubwa la ukosefu Wa ajira  .Hali hii imekuwa mbaya zaidi katika nchi zilizopo chini ya jangwa la sahara ikiwemo Tanzania.Kwa sababu hiyo basi kumekuwa na wimbi kubwa la vijana wenye elimu na wasio na elimu ambao wako mtaani bila kazi .

Lakini ukweli unabaki palepale kuwa kama hakutakuwa na uwajibikaji kutoka kwa mtu binafsi mpaka ngazi ya Taifa tatizo hili litaendelea kuwa vile vile na zaidi litaendelea kuwa sugu .

Nimeona hivi karibuni TCU ikifuta baadhi ya vyuo vikuu wakidai kuwa havina sifa lakini mimi nadhani ni mpango wa serikali wa kupuguza idadi ya wasomi wengi walioko mtaani .
Uwepo wa wasomi wengi mimi naona siyo tatizo swala ni kwa jinsi gani wasomi hawa wamejengwa katika misingi ya uwajibikaji na uwezo kutumia elimu zao kwa vitendo kuliko kujengwa katika misingi ya kumaliza na kuanza kuzungusha bahasha.

Kama mtu binafsi atajua wajibu wake na kuachana na mitazamo ya ubaguaji wa kazi  tatizo la ajira halitakuwepo .Shida ni kwamba wasomi wengi hawataki kuwajibika kwa kutumia nguvu zao wenyewe na mawazo yao wanataka kufuata mawazo ya mtu na kujenga ndoto ya mtu .Msomi yuko radhi kwenda ofisini ili jamii tu ione kama naye anaamka asubuhi kwenda ofisini akifika huko yeye kazi yake ni kuchat tu na kusubiri muda wa kurudi  nyumbani .Kuna mahali niliwahi fanya kazi na mtu wa jinsi hii ambaye muda mwingi kazini aliutumia kuchat sana huku akisubiri muda wa kurudi nyumbani na mshahara mwisho wa mwezi tu .

Unaweza kukuta pia wanafunzi wanamaliza vyuo na kutafuta kazi zaidi ya miaka mitatu bila mafanikio wakati kwa muda huo wa kusubiri kazi mwanafunzi huyo anakuwa na uwezo wa kuanzisha hata biashara ndogo na akaweza kuishi na kukuza uchumi wake binafsi pamoja na pato la taifa kwa ujumla .Vijana Wameshindwa kuelewa kuwa kitu cha kwanza na cha muhimu katika maisha sasa ni kuwa na wazo zuri  na kama mtu ana uwezo mkubwa wa kuona fursa tatizo la ajira litaisha na vijana hawatailalamikia serikali au mtu yeyote.Vijana wamekua wavivu wa kufikiri na kusubiri miujiza itokee jambo ambalo halitakuja kutokea hapa chini ya Jua

Familia kwa upande mwingine wana wajibu wa kuwajibika katika kuandaa na kuwwajenga watoto wao katika misingi ya kujiajiri .Utashangaa mtu anamaliza chuo halafu familia inamuuliza " umeshaanza kuandika barua za kuomba kazi??? " badala ya kuuliza " una wazo gani tukupe mtaji ?" .Familia zinapaswa kuondokana na dhana ya ajira  na kuamini kuwa hata mtu akiamini kujiajiri anaweza kufika mbali .Kama wazazi wameajiriwa wasitamani watoto wao waje waajiriwe .Kama kila familia itaweza kuzalisha ajira tatizo la ajira halitabaki kuwa kama lilivyo.

Asasi za kidini zina mchango mkubwa katika kuondoa tatizo hili la ajira kwa kuanzisha miradi mbalimbali ambayo itaajiri waumiini wake .Shida ni kwamba Dini sasa zimekuwa kama biashara badala ya kubadili maisha ya watu na waumini pia wamekubali miujiza kuliko uhalisia wa jambo .

Nimalize kwa kusema kuwa tatizo hili litamalizwa na mimi na wewe kwa kuangalia namna ya kuzalisha ajira ambazo zitaajiri watu kuliko kuendelea kulaumu serikali wakati sisi wenyewe ni vyanzo vya ukosefu wa ajira kwa watu maana tumeshindwa hata kuanzisha genge na kumuweka mtu walau apate elfu moja kwa siku.

Joas (JYB) 0753836463