![]() |
Pata kitabu hiki kwa bei ya sh elfu tano tu (5,000/= 0713804078 |
1
USIANZE
MPAKA UWE NA TAARIFA ZA KUTOSHA
Wengi huanzisha
biashara kwa kuwaiga watu wao wa karibu na huanza bila kufanya utafiti wa
kutosha kuhusiana na hizo biashara. Yawezekana hufanya hivyo kwa kuwaiga tu
wale wanaofanya au wamewaona watu fulani wakiwa wanafanya nao wakaamua kujiunga
nao.
Kuna wakati Bwana Yesu
akiwa anafundisha akawaeleza wanafunzi wake kuwa mtu yeyote akitaka kujenga mnara
ni muhimu akae chini na kupiga hesabu (cost calculation) kama anavyo vya kuumalizia? asije
kuishia katikati na watu wakaanza
kumcheka kuwa alianza kwa kasi sasa kasi yake ipo wapi, rejea kitabu cha Luka
14:28-30.
Maana yake kabla
hujafanya kitu chochote ni lazima uketi chini (utulie) na kupiga hesabu (kuwa
na mipango na mikakati ya kueleweka) na ndipo mtu aweze kuanza anachoanza. Kama
mtu hatoweza kufanya hivyo ni dhahiri ataanza ila hatoweza kufika mahali
popote.Wapo vijana wengi
sana ambao wanajihusisha kufanya vitu ambavyo hawana taarifa navyo kabisa.Usianze kufanya mpaka
umepata taarifa za kutosha.
Wakati namaliza chuo
mwaka wa tatu kila mmoja alikuwa katika mchakato wa kutafuta sehemu ambayo
atafanya kazi ya kumpatia kipato kizuri, wengi walijihusisha na kufungua
taasisi (CSOs)
kutokana na taarifa ambazo zilikuwa
zikienea kuwa mkiwa na CSOs yenu serikali itakuwa inatoa ruzuku ya kuanzia na
wengi wakaamua kuanzisha hizo taasisi lakini baada ya muda mfupi tu taasisi
zile zilikufa na kubakia kwenye makaratasi. Watu walikuwa na shauku ya
kuanzisha ila maarifa ndio ilikuwa tatizo.
Tafuta taarifa kwa
kadri uwezavyo, fuatilia watu mbali mbali waliowahi kufanya na uwaulize ili
upate taarifa zitakazokusaidia nawe kufanya kwako.
Nyakati za hivi
karibuni kumetokea wimbi kubwa la ufugaji wa sungura na ilipotangazwa kuwa
katika kufuga sungura kuna faida kubwa wapo watu wengi sana wakakimbilia kufuga
sungura ili kuuza nje ya nchi ila matokeo yake yalionekana kuwa wengi walifanya
ila wakapata faida kidogo na wengine hawakupata kabisa kwa sababu tu walifanya
ila hawakuwa na taarifa za kutosha.
Mwaka 2016
tulishuhudia wimbi kubwa la wakulima wa nyanya wakipata hasara kubwa sana kwa
kuuza tenga moja shilingi 700/= na wengine kuona ni bora wakawapa ng’ombe na
nguruwe wakala kuliko hasara waliyoipata. Suala kama hili wengi waliishia
kuilaumu serikali kuwa haijawatengenezea mazingira ya soko na viwanda rafiki
vya zao hilo kama vile vya usindikaji. Nina uhakika kama wangeuza shilingi 50,000/=
kwa tenga, hizi lawama tusingezisikia. Ukitafakari utagundua wengi hufanya
kilimo kwa ufinyu wa taarifa na sio watafiti kabisa, na wengi huwa wanapigia
mahesabu faida wanayopaswa kuipata na huwa hawana tahadhari ya upande hasi.
Wengi walilima nyanya kwa sababu walisikia rafiki au ndugu zao wakiwaambia
kilimo cha nyanya kinalipa sana.
Katika eneo hili ni
muhimu sana kuzingatia upataji wa taarifa za kutosha kabla ya kuanza. Ukiona
watu wengi wanajihusisha na kulima matikiti ni lazima ufahamu kuwa matikiti
yanakwenda kushuka bei sokoni kwa kuwa yatakuwa yanapatikana kwa wingi zaidi,
na ndicho kinawakumba watu wanaambiwa wakilima zao fulani lina faida sana na
unakuta karibia wote wanaingia huko na kusahau mazao mengine. Ukweli ni kuwa
kila zao linalipa ila inategemea unafanya kwa namna gani.
Nimeona watu wengi
sana wakiigana bila hata ya kuwa na taarifa, yaani kila mtu anataka kufanya
kitu kile kile anachofanya mwingine mwisho wa siku wanaofanya biashara za namna
hiyo wanakuwa wengi na kupoteza kabisa soko. Kabla hujaanza piga hesabu na
usifanye kwa sababu fulani anafanya, wewe fanya kwa kuwa unaona unamudu kufanya
hiyo biashara.Kuna nyakati watu
wengi walifanya kwa kuigana kuanzisha biashara za m-pesa, tigo pesa, airtel
money na baada ya muda mfupi wengi wakaanza kuacha na kurudi nyuma na kuona ni
biashara ngumu kwa sababu hawakupiga hesabu. Wengine walikuwa wakikosa wateja
maana mabanda yakawa mengi kuliko huitaji.
Duniani hakuna kitu
kigumu wala kitu kirahisi, ugumu au rahisi wa kitu unategemea na mtu mwenyewe.
Kile unachokiona kigumu sana kuna mwingine ndicho anaona ni rahisi zaidi na
kile unachokiona kirahisi kuna mtu anakiona ni kigumu sana. Ni wewe ndiye
unaweza kufanya biashara yako, kampuni yako, na taasisi yako vionekane vigumu
kutekelezeka au vikawa vyepesi.Taarifa za juu juu
zinasababisha wengine kuwa na matarajio ya juu sana ‘too much expectations’ na
mambo yanapowageukiwa na kuwa ndivyo sivyo hujikuta katika hali ya kukata tamaa
na kuamua kuachana na vile walivyovianzisha.
2
USISHINDANE NA MTU, SHINDANA NA MAONO YAKO
Watu wengi hupenda mashindano, na mambo mengi sana hufanyika kwa
mashindano. Mashindano hayo hupelekea wivu na wakati mwingine chuki na maneno
mabaya haswa pale mshindanaji anapohisi kushindwa. Watu waliofanikiwa na
wanaofanikiwa duniani kote ni watu wanaohangaika kutekeleza maono yao usiku na
mchana na si watu wa kuhangaika kushindana na wengine, na ni nadra sana
kuwakuta wakizungumzia watu wengine kwa namna ya kuwakosoa ili wao waonekane ni
bora zaidi ya hao watu. Ukiwakuta wanafuatilia watu wengine hufuatilia kwa
kutaka kujifunza na kuhamasika na si kutaka kuiga.
Ni jambo la kawaida sana ukamkuta mtu ameamua kununua gari kwa sababu
rafiki yake amenunua na anashindwa kuangalia vipaumbele. Simaanishi kununua
gari ni tatizo, tatizo ni kukosa vipaumbele vya msingi. Au ukamkuta mtu
anakosoa kazi ya mwingine ili tu yeye aonekane ni bora zaidi ya huyo mtu.
Usishindane na mtu maishani mwako, hujui huyo unayeshindana nae ametokea
wapi, na anaelekea wapi, kamwe usiige mwendo wa mwenzio lakini hamasika kwenye
mwendo wa mwenzio. Kila mtu anamwendo wake na ana sehemu anayopaswa kufikia,
mara zote hangaikia kufika kwenye ule mwendo unaopaswa kufikia.
Wakati nasoma chuo kikuu cha Dar es salaam nilikuwa na rafiki yangu ambaye
pia alikuwa ndiye katibu wangu nami nikiwa mwenyekiti katika fellowship ya
kuabudu pale chuoni. Kila siku tulipokuwa tukimaliza ibada alisalimia watu na
kisha kuondoka, alikuwa anatembea mwendo wa kasi sana na wakati mwingine
ulikuwa ukitaka kuongozana nae ungemuacha tu akutangulie kwa sababu kasi yake
ilikuwa kubwa akiwahi majukumuni mwake, nafikiri alifahamu vyema sana kuwa kuna
majukumu yanamsubiri sehemu fulani na ndiyo maana alikuwa akifanya upesi
kuyaelekea. Ule mwendo ulikuwa mgumu sana kwa wengi kwa kuwa kama ungetaka
kumuiga mngeweza kufika lakini ukiwa umechoka ila yeye asingechoka kama wewe
kwa kuwa anaumudu na ndio mwendo wake, na pia mkifika unaweza ukajikuta hata
viatu vyako vipo katika hali mbaya kwa sababu ulitembea katika mwendo ambao
siyo wako. Ni vyema ukajifunza kutembea katika mwendo wako katika ustadi na
unadhifu huku ukijua ni wapi unaelekea.
Kuna mtu aliyekuwa
ameamka kufanya mazoezi ya asubuhi kwa kukimbia barabarani, wakati anakimbia
aliona mtu mbele yake akiwa amemuacha mbali sana, akaamua kuanza kumfukuzia,
alimfukuzia mpaka akamkuta, alipomkuta akazidi kukazana hata alipompita kabisa
ndipo alipojisikia vyema na baada ya kukimbia tena umbali mdogo akaona yule mtu
anakata kona anaingia nyumbani kwake kwa maana ameshafika mwendo wake, naye
akawa amebakia peke yake barabarani.
Fahamu ya kuwa kila mtu ana mwendo wake na ana kituo chake anachopaswa
kwenda, usiige mwendo wa mwenzio na wala usishindane nae, ila waweza kuhamasika
kwa namna anavyotenda.Usimkosoe mtu ili wewe uonekane ni bora zaidi yake. Kuna ambao huamini kuwa
wakiwapaka wengine matope basi hujisafisha na kuwa safi, ila ukweli ni kuwa mtu
bora ni bora tu hata ukimpaka matope atang’aa tu.
Na huwezi kuwa bora kwa kukosoa walio bora au kuwa bora kwa kushindana na
walio bora ila unaweza kuwa bora kwa kuwapenda, kuwakubali, kujifunza kwao na
kuwa karibu nao.
Usishindane na mtu maishani mwako, mara zote angalia kusonga mbele na
tafuta mambo yatakayokufanya kuwa bora na usonge mbele daima ili utimize
malengo uliyojiwekea.Maono yako katika kitu ulichokianzisha ni ya muhimu sana zaidi ya
kushindana na watu. Wakati wote palilia na kuyaatamia maono yako.Hii Ndiyo Kanuni:
·
Macho yako
yatazame picha ya ndani siku zote ya kule unakoelekea
Ukiwa na picha ya taasisi, biashara, kampuni yako inavyopaswa kuwa basi ni
muhimu macho yako yaitazame ile picha zaidi ya picha iliyopo sasa katika
mazingira yaliyokuzunguka. Kama hauna picha ya kule unapoelekea basi inakuwa
rahisi sana kuchanganywa na yale unayoyaona sasa katika mazingira yako sasa.
Kama unafanya uzalishaji wa chillsource uwe na picha ndani yako kuwa siku
moja lazima nije kuwa na kiwanda kikubwa Tanzania, Afrika na Ulimwenguni
ambacho kitakuwa kinajihusisha na uzalishaji wa biashara hiyo. Au kama unashona
nguo kuwa na picha ya kuja kumiliki kiwanda kikubwa cha ushonaji kuanzia nchini
mpaka nje ya nchi na ndicho kitu muhimu zaidi kukifanyia kazi usiku na mchana.
Ona mbali zaidi ya mambo yako ya sasa yanavyoonekana, usiwe na uonaji
unaodhibitiwa na mazingira yaliyopo. Hata kama unatumia brenda kuzalisha juisi
unayozalisha sasa, tazama kama mtu ambaye anajua kuwa hajafika. Endelea kuona
kuwa siku moja wewe utakuwa ni mtu anayezalisha juisi nzuri zaidi ya
wazalishaji wote tulionao leo.
Ijapokuwa mwanzo wako ni mdogo inawezekana mwisho wako utakuwa mkubwa.
Fanyia kazi ile picha unayoiona na usihangaike na mashindano na watu
unaowaona. Kataa kuongozwa na maisha ya wengine, maisha yako yaamriwe na
kuongozwa na aina ya maono uliyonayo kwa sababu kila mtu anamwendo wake.
Usiige miendo ya watu kuna wengine hawaendi mbali kama unapoelekea wewe na
ndio maana wanatembea taratibu, ukiiga unadhani eti mnachelewa wote kumbe
unayechelewa ni wewe. Kuna wengine muda wao wa kufika ni saa saba japo wameanza
safari mapema zaidi usijidhanie kuwa uko nao wewe wa saa sita piga mwendo zaidi
yao.
Wengi sana hupenda kufanya kama fulani anavyofanya kwa kudhania huo ndio
mfumo wa marafiki. Kataa hali ya namna hiyo, kila mmoja ana maono yake. Toa
kipaumbele kwenye mambo ya msingi tu yatakayokufanya ufikie yale malengo
uliyonayo.
·
Masikio yako
yasikilize sauti ya kule unapoelekea zaidi.
Kuna tofauti kati ya kusikia na kusikiliza, unaweza ukasikia lakini
ukashindwa kusikiliza.
Yape masikio yako kusikiliza sauti ya maono yako japo yatasikia sauti
nyingi ila yape kusikiliza (umakini) ile sauti ambayo imebeba kesho yako.Ukiyapa kusikiliza yanayotokana na mazingira uliyopo sasa yanaweza kupeleka
taarifa ya kukatisha tamaa katika moyo.
Watu wanaweza kukusemea wewe kwa vile unavyoonekana leo ila sauti ya ndani
ndiyo inaweza kukutambulisha wapi unaelekea, usiishie kwenye wigo wa watu
wanavyoona, ona kwa jicho la ndani lionalo maono yako.Wakati fulani nilitafuta mshauri (mentor)ili anisaidie ushauri wa ndani
kuhusiana na shughuli ninazozifanya katika kampuni yangu ya Gracious Printing
Press. Nilipokutana naye nilimuelezea kule napopaswa
kufikia na aina ya hatua ambazo nimekuwa nikichukua ili kufikia, aliposikia
akanitazama kwa muonekano wa nje na kuona sitoweza kufika haswa kama nitafanyia
biashara hapa Dar es salaam, akaona anishauri nifanye biashara nyingine na kama
nafikiria aina ya biashara hii ni lazima nifikirie kutoka nje ya Dar es salaam
ambapo hakuna ushindani mkubwa.
Alichoona labda sitoweza ushindani uliopo Dar es
salaam, lakini mimi nilikuwa naona kampuni kubwa sana na naamini kwenye
ushindani wa kibiashara ndipo kwenye ubora na mafanikio na ndiyo sehemu ambapo
akili hufanya kazi zaidi ya kawaida. Nilimsikiliza ila nilipoona ushauri wake
unakinzana na safari yangu nikaona niendelee mbele tu kiutendaji.
Pata Mengi
kupitia Kitabu chake kinachoeleza kwa kina Mpigie
Kelvin Kitaso kwa namba hizi 0713804078 bei ni shillingi elfu tano tu (5,000/=)